Na Mwandishi Wetu
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Mwadhamu Polycarp Kardinali Pengo kilichotokea usiku wa Februari 19, 2026 jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari Machumu, imeeleza kuwa Rais Samia amepokea kwa masikitiko taarifa za kifo hicho.
Rais Samia alimwelezea Kardinali Pengo kama kiongozi wa kiroho na mzalendo aliyetoa mchango mkubwa katika kuimarisha imani, maadili, umoja na mshikamano wa kitaifa.
Amesema taifa limepoteza kiongozi aliyelitumikia kwa uadilifu na kujitolea kwa muda mrefu kupitia nafasi mbalimbali ndani ya Kanisa Katoliki.
“Taifa limepoteza kiongozi aliyelitumikia kwa uadilifu na kujitolea, na mchango wake katika malezi ya kiroho na maadili utaendelea kukumbukwa, kuthaminiwa na kuenziwa,” sehemu ya taarifa hiyo ilieleza.
Aidha, Rais Samia alituma salamu za pole kwa Mheshimiwa Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), viongozi wa dini, waumini wa Kanisa Katoliki pamoja na Watanzania wote kwa ujumla walioathiriwa na msiba huo.
Rais aliwahimiza Watanzania kuendelea kuwa na moyo wa subira katika kipindi hiki cha majonzi na kumuomba Mwenyezi Mungu aipumzishe roho ya marehemu mahali pema peponi.


