Na Mwandishi Wetu
KLABU ya Simba imeliandikia barua Jeshi la Polisi ili kuwachukulia hatua za kisheria wanachama na mashabiki wa klabu hiyo waliohusika na mkutano wa kutoa kashfa na maneno yasio ya staha kwa mwekezaji wao Mohamed Dewji (Mo).
Kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa na Klabu hiyo, Bodi ya Wakurugenzi ya Simba imesikitishwa na vitendo hivyo na kutaka wote waliohusika au kula njama za kuandaa mkutano huo kufikishwa katika vyombo vya dola kwa makosa ya jinai.
“Bodi inasisitisha kuwa haitabariki wala kuvumilia mtu yoyote anayeharibu taswira ya klabu kwa namna yoyote ile,” imesema taarifa hiyo.
Aidha uongozi wa Simba, umetoa onyo kwa baadhi ya wanachama na mashabiki wa klabu hiyo wanaotumia nembo rasmi ya klabu bila kupata ruhusa ya moja kwa moja kutoka kwa ngazi za juu za klabu hiyo.
Umetoa wito kwa wanachama na mashabiki kuzingatia taratibu rasmi za klabu na kushirikiana kwa pamoja katika kuendeleza heshima na hadhi ya klabu.



