Na Winfrida Mtoi
Kuelekea mchezo wa Ngao ya Jamii kesho Septemba 16,2025, makocha wa Simba na Yanga, Fadlu Davids na Romain Folz, kila mmoja ametambia ubora wa wachezaji wake katika kukabiliana na michezo migumu, huku wakijivunia maandalizi waliyofanya kuwa ndiyo yatakayoamua matokeo ya mchezo huo wa ufunguzi wa msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Mchezo huo utapigwa katika dimba la Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam, majira ya saa 11:00 jioni, mwenyeji akiwa Yanga ambaye ndiye bingwa mtetezi.
Akizungumzia mchezo huo mbele ya waandishi wa habari leo, Kocha Mkuu wa Yanga, Folz, ambaye ni mara yake ya kwanza katika dabi ya Kariakoo, ameweka wazi kuwa wamejiandaa vizuri kimwili, kiakili na wana shauku ya kupata matokeo mazuri.
Folz amesema wanakwenda kucheza mechi kubwa yenye presha na wanatakiwa kuwaheshimu wapinzani kutokana na kuwa wana timu nzuri, lakini watahakikisha wanawapa mashabiki wao kile wachohitaji.


“Ni mechi ya kuanza msimu tunakwenda kucheza mbele ya mashabiki wetu, nina kundi kubwa la wachezaji wazuri ambao wanaweza kumudu mazingira ya mchezo wowote. Utakuwa ni mchezo mzuri tutacheza katika kiwango bora ili kuwafurahisha mashabiki wetu,” amesema.
Kwa upande wake kocha wa Simba, Fadlu ameeleza kuwa hana presha ya mchezo huo, tayari ana uzoefu wa dabi tofauti na benchi la ufundi la wapinzani wao ambalo ni jipya, hivyo wanachohitaji ni kutwaa taji hilo kwa ajili ya mashabiki wao.
“Wachezaji wangu wana morali ya mechi hii kubwa na wapo tayari kuhakikisha wanapambana na kupata ushindi ambao utakuwa muhimu kwetu kwa kuanza msimu na taji la kwanza. Ni kipimo kizuri baada ya maandalizi ya msimu,” amesema.
Wakati huo huo mwamuzi wa kati wa mchezo huo ametangazwa na Shirikisho la Soka Tanzani (TFF), kuwa ni Ahmed Arajiga kutoka Manyara, atasaidiwa na Mohammed Mkono na Kassim Mpanga, wakati mwamuzi wa akiba Ramadhan Kayoko.