Chalamila awaalika wakazi wa Dar kujitokeza kwa wingi uzinduzi wa Kituo cha biashara cha EACLC

Na Tatu Mohamed

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amewaalika Watanzania na wakazi wa Jiji hilo kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye hafla ya uzinduzi wa Kituo Kikubwa cha Biashara na Usafirishaji (EACLC), utaofanyika Agosti 1, 2025 katika eneo la zamani la Stendi Kuu ya Ubungo.

Chalamila amesema uzinduzi huo utafanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye atakuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo ya kihistoria.

“Nitoe wito kwa wananchi wote, wafanyabiashara waliokwisha chukua maduka, wale wanaotarajia kuchukua, na wote wanaopenda maendeleo ya biashara nchini, wafike kushuhudia tukio hili muhimu. Ni uzinduzi wa kituo ambacho kitabadilisha taswira ya biashara si tu Tanzania, bali Afrika Mashariki kwa ujumla,” amesema Chalamila.

Ameeleza kuwa kituo hicho kikubwa kimejengwa katika eneo ambalo awali lilikuwa Stendi ya Ubungo, baada ya serikali kuhamishia shughuli hizo Mbezi.

“Katika eneo hilo, serikali kupitia Mamlaka ya Uwekezaji kwa kushirikiana na wawekezaji kutoka China, imefanikisha ujenzi wa kituo cha kisasa cha kibiashara.

“EACLC ni mradi wa kimkakati uliogharimu zaidi ya dola milioni 100. Kina maduka zaidi ya 2,000, maghala ya kisasa, sehemu za ofisi, maegesho ya magari, na huduma nyingi nyingine za kibiashara zinazopatikana kwa kukodishwa kwa Watanzania na hata wageni kutoka nje,” alifafanua.

Amesema Kituo hicho kilianza kujengwa Mei 2023 na sasa ujenzi wake umekamilika.

Chalamila amesema ujenzi huo ni ishara ya dhamira ya serikali kuendeleza mazingira ya biashara na uwekezaji nchini, huku akisisitiza kuwa uwekezaji huo haujachukua nafasi ya wafanyabiashara wazawa bali ni mfumo wa ubia unaowanufaisha wote.

Ametoa wito kwa wawekezaji wengine kufika kwenye Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi kupata taarifa sahihi za jinsi ya kuwekeza nchini.

spot_img

Latest articles

Mwanamke ashikiliwa  Polisi kwa  kumuua mume wake na kumfukia ndani ya nyumba yao

Na Mwandishi Wetu Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita linamshikilia mwanamke mmoja aliyefahamika kwa jina...

Padre aliyepotea apatikana akiwa hai

Na Mwandishi Wetu Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma limefanikiwa kumpata Padre Camillus Nikata wa Jimbo...

Waangalizi wa Uchaguzi watakiwa kutoingilia mchakato wa Uchaguzi Mkuu

Na Mwandishi wetu, Dodoma WAANGALIZI wa Uchaguzi wa ndani na wa kimataifa wametakiwa kuzingatia sheria...

More like this

Mwanamke ashikiliwa  Polisi kwa  kumuua mume wake na kumfukia ndani ya nyumba yao

Na Mwandishi Wetu Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita linamshikilia mwanamke mmoja aliyefahamika kwa jina...

Padre aliyepotea apatikana akiwa hai

Na Mwandishi Wetu Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma limefanikiwa kumpata Padre Camillus Nikata wa Jimbo...

Waangalizi wa Uchaguzi watakiwa kutoingilia mchakato wa Uchaguzi Mkuu

Na Mwandishi wetu, Dodoma WAANGALIZI wa Uchaguzi wa ndani na wa kimataifa wametakiwa kuzingatia sheria...