Na Mwandishi Wetu
Sakata la Klabu ya Yanga la fedha za zawadi, limeendelea baada ya kutoa tuhuma nyingine kwa Shirikisho la Soka Tanzania( TFF) ambapo leo Juni 10, imelijibu shirikisho hilo juu ya madeni na kusema kwa misimu mitatu mfulululizo haijawahi kulipwa fedha yoyote ya ubingwa wa Kombe la Shirikisho, kuanzia msimu wa 2021/22, 2022/23 na 2023/24.
Yanga imetoa taarifa hiyo muda mfupi baada ya TFF kujibu kauli ya Ofisa Habari wa Klabu hiyo, Ally Kamwe ambaye jana alisema hawatacheza fainali ya Kombe la Shirikisho msimu huu kwa sababu haijapewa fedha za zawadi za ubingwa wa msimu uliopita.
Kutokana na kauli hiyo ya jana, wadhamini wa mashindani hayo, benki ya CRDB ilitoa taarifa kuwa tayari walishailipa TFF fedha hizo zawadi ya msimu uliopita.

Hali hiyo iliibua TFF leo Juni 10, 2025 na kujibu tuhuma kuwa fedha walizotakiwa kulipwa mabingwa hao zimefidia malipo ya klabu hiyo iliyotakiwa kulipa ikiwamo kulipia ada za wachezaji wa kigeni wa timu hiyo.
“Tumesikia Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga kupitia vyombo vya habari akidai kuwa klabu yao inaidai TFF Tsh 200,000,000(Milioni mia mbili) ambayo ni zawadi ya ubingwa wa kombe la shirikisho la benki ya CRDB.

“Tunapenda kutoa ufafanuzi kuwa TFF ndiyo inayoidai klabu ya Young Africans, iliomba kwa barua fedha hizo za zawadi katika mashindano mbalimbali zikatwe kulipia malipo wanayotakiwa kulipa kwa TFF ikiwemo ada za wachezaji wa kigeni.
Hata hivyo Yanga haijamezea hali hiyo, kwani imeibuka na taarifa mpya ya leo Juni 10,2025, ikidai hakuna uthibitisho wowote wa kimaandishi unaoonesha kama TFF wamewahi kulipa fedha hizo za ubingwa kwa klabu Yanga.

“Ieleweke ada za malipo ya wachezaji wa kigeni walizozisema kwenye taarifa yao, hulipwa mwanzo wa msimu mpya na hela hizi za ubingwa hutolewa mwisho wa msimu. Klabu ya Young Africans haijawahi kupokea taarifa yoyote rasmi kutoka TFF kuhusu klabu yetu kuwa na deni kwao,” imesema taarifa ya Yanga.