Na Mwandishi Wetu
Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), imeahirisha mchezo Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya Simba na Dodoma Jiji uliopangwa kuchezwa Februari 15, 2025 katika Uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa ya bodi hiyo, kuahirisha mchezo huo kumetokana na hali ya kiafya ya maofisa na wachezaji wa Dodoma Jiji kutokuwa nzuri baada ya ajali ya basi waliyopata wakati wakisafiri kutokea Ruangwa mkoani Lindi.
“Ajali hiyo imesababisha athari hasi kwa klabu ya Dodoma Jiji kwa kuchelewesha safari yake ya kuelekea mkoani Dar es Salaam pamoja na kuathiri maandalizi ya kiufundi kwa kuwakosa wachezaji na maofisa wa ufundi ambao walipata majeraha katika ajali hiyo. Bodi itatangaza tarehe mpya ya mchezo huo hivi karibuni,” imesema taarifa hiyo.
Aidha kwa upande wa taarifa ya klabu ya Dodoma Jiji, kikosi hicho kimewasili salama jijini Dodoma na ambapo taratibu za kitabibu zitaendelea kwa majeruhi wote katika Hosptali ya Benjamin Mkapa.
Dodoma Jiji ilipata ajali Februari 10, 2025 baada ya basi walikuwa wakisafiria kutumbukia mtoni katikati ya Nangurukuru na Somanga.