Mgombea nafasi ya uenyekiti chama cha ACT Wazalendo, Juma Duni Haji (babu Duni) ameamua kujiondoa kwenye kinyanganyiro hicho, ikiwa ni siku moja kabla ya uchaguzi wa mwenyekiti wa chama hicho cha upinzani nchini.Babu Duni amejiondoa katika kinyang’anyiro hicho leo Jumatatu, Mach 4, 2024 wakati akizungumza na wajumbe wa Halmashauri Kuu Taifa ya ACT – Wazalendo katika ukumbi wa Hakainde Hichilema uliopo makao makuu ya chama hicho, Magomeni jijini Dar es Salaam.
Duni ambaye alikuwa akigombea kuteteta nafasi yake, amesema ameamua kujiondoa kwenye kinyang’anyiro hicho na kumuunga mkono aliyekuwa mshindani wake pekee, Othman Masoud Othman. Hivyo Othman amebaki kuwa mgombea pekee.
Uamuzi huo wa Babu Duni umekuja saa chache bada ya kuwapo malalamiko yake juu ya kuwapo hujuma za watu waliokuwa wanamshinikiza kujitoa katika kinyang’anyiro hicho kwa madai kwamba ni mzee, huku kukiwa na taarifa za wenyeviti kadhaa wa mikoa kumchukulia fomu mshindani wake.Hata hivyo, leo, Babu Duni amesema amelazimika kujiondoa baada ya kutafakari kwa kina akijua kuwa chama hicho kina malengo makubwa ya kushika dola, hivyo kubaki kwake bila shaka kungekiletea madhara.
“Nimeamua kujiondoa kuweka heshima kwenye chama kwa sababu tuna muda mfupi kuelelea kwenye uchaguzi, hatuhitaji msuguano,” alisema
Babu Duni, huku akiwataka viongozi wakuu wa chama hicho watakaochaguliwa kutowatenga kabisa wale wote ambao walikuwa wakimuunga mkono kwenye kampeni zake.Katika hatua nyingine, mgombea nafasi makamu mwenyekiti Zanzibar, Hijja Hassan Hija naye amejiondoa kwenye uchaguzi huo kKpitia barua yake iliyosomwa na Katibu Mkuu, Ado Shaibu, akisema haoni sababu ya kuendelea kugombea, hivyo kumwachia Ismail Jussa Ladhu awe mgombea pekee.