Riyadh, Saudi Arabia
NAIBU Waziri wa Madini, Dk. Steven Kiruswa, amesema Tanzania imetambua shughuli za uongezaji thamani madini kama nguzo muhimu ya kuleta maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii lengo kubwa ikiwa ni kuondokana na uuzaji na usafirishaji wa madini ghafi kwa nchi zinazozalisha madini mbalimbali barani Afrika.
Amebainisha hayo wakati akizungumza katika Kongamano la Kimataifa la Madini lijukanalo kama ‘Future Minerals Forum 2026’ lililowakutanisha mawaziri, viongozi mashuhuri na wadau wa sekta ya madini kutoka zaidi ya nchi 100 ndani na nje ya Bara la Afrika.
Dk. Kiruswa amesema kuwa, rasilimali madini ni moja ya utajiri mkubwa uliopo barani Afrika hivyo kuna umuhimu mkubwa wa kuweka mkazo katika shughuli za uongezaji thamani madini ndani ya nchi za Afrika ambapo kama kila nchi itazingatia hilo itakuwa moja ya ufunguo wa kubadilisha utajiri wa madini kuwa kichocheo cha maendeleo endelevu kwa wananchi na taifa kwa ujumla.

Akielezea kuhusu juhudi mbalimbali zinafanywa na Serikali ya Tanzania katika kuendeleza Sekta ya Madini, Dk. Kiruswa amesem kuwa Serikali ya Tanzania inaendelea kuboresha miundombinu ya usafirishaji na mawasiliano ikiwemo ujenzi wa reli ya mwendo kasi, barabara, nishati ya umeme na uongezaji wa bandari ili kuhakiskisha rasilimali zinasafirishwa kwa urahisi kutokea mgodini na kiwandani.
Amefafanua kuwa, ili kufanikisha hilo ni vyema kila taifa liendeleze viwanda vya uchakataji, uchenjuaji na usafishaji madini akitolea mfano kwa taifa la Tanzania linavyoendeleza juhudi mbalimbali katika mnyororo wa thamani madini ikiwemo kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji, mifumo ya usafirishaji katika ngazi ya kimataifa kupitia Bandari ya Dar es Salaam.
Amesisitiza kuhusu ushirikiano wa kikanda ndani ya Bara la Afrika kwa kuanzisha vituo vya kikanda vya uchenjuaji, uchakataji na usafishaji madini katika nchi zenye miundombinu mizuri ili nchi jirani pia ziweze kuvitumia ikiwa pamoja na kujenga mahusiano ya kisekta kati ya Afrika na Muungano wa kiuchumi na kikanda kati ya nchi za Afrika na nchi za Mashariki ya Kati.


