Na Mwandishi Wetu
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limemthibitisha Dk. Mwigulu Nchemba, kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania akichukua nafasi ya Kassim Majaliwa.
Mwigulu amethibitishwa leo Novemba 13, 2025 kwa kura za ndio 369 kati ya kura 371 zilizopigwa huku za hapana hakuna na zilizoharibika zikiwa ni mbili.
Uthibitisho huo wa Bunge ni baada ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kumteua Mwigulu ambaye ni Mbunge wa Iramba Magharibi, Mkoani Singida, pia alikuwa Waziri wa Fedha katika kipindi kilichopita.
Akitoa hotuba ya shukrani baada ya kuidhinishwa bungeni jijini Dodoma, Waziri huyo mteule, , amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoingia katika awamu yake ya pili ina kazi kubwa ya kusimamia utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025–2050, ambayo inalenga kuleta mafanikio makubwa ya kiuchumi na kijamii nchini.
Amesema Dira hiyo inaweka kipaumbele kwenye masuala ya ajira, ambapo lengo ni kutoa ajira milioni nane kwa vijana nchini.
Ameeleza kuwa anatambua changamoto ya ajira kwa vijana na ameahidi kushirikiana kwa karibu na Rais Samia Suluhu Hassan kuhakikisha ajira zinapatikana na umasikini unaokadiriwa kufikia asilimia 26 unapungua kwa kiwango kikubwa.


