Na Mwandishi Wetu
Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Taifa, Tundu Lissu, amerejeshwa mahabusu leo na anatarajiwa kurejea Jumatatu Septemba 15, 2025 kwa ajili ya Mahakama kutoa uamuzi juu ya mapingamizi aliyowasilisha kuhusu kesi ya uhaini inayomkabili.
Kesi hiyo imesikilizwa siku nne mfululizo tangu Jumatatu katika Mahakam Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Dar es Salaam mbele ya jopo la Majaji watatu, wakiongozwa na Jaji Dustan Nduguru akisaidiana na Jaji James Karayemaha na Ferdinand Kiwonde.
Tayari Lissu amekamilisha mawasilisho ya mapingamizi yake leo Septemba 11, 2025, madai ya msingi ikiwa ni mchakato wa kesi hiyo katika Mahakama ya Kisutu ulikuwa na makosa mengi na kutaka kesi ifutwe, aachiwe huru, hivyo kinachosubiriwa ni uamuzi kutoka kwa jopo la Majaji watatu.
Iwapo Mahakama Kuu itakubaliana na hoja za Lissu, kesi hiyo inaweza kufutwa rasmi, endapo hoja zikikataliwa basi itaendelea kusikilizwa kwa mujibu wa taratibu za kisheria.
Akizungumza na waandishi wa habari nje ya mahakama hiyo, Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika amesema wakati dunia itakuwa inaadhimisha Siku ya Demokrasia, kwao itakuwa tofauti kwani watakuwa mahakamani kujua hatma ya kesi ya Mwenyekiti wao.