Na Mwandishi Wetu
Jeshi la Polisi Tanzania limetangaza msamaha wa kutokushtakiwa kwa wananchi wote wanaomiliki silaha kinyume cha sheria endapo watasalimisha silaha hizo kwa hiari kuanzia Septemba 1 hadi Oktoba 31, 2025.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Msemaji wa Jeshi la Polisi Makao Makuu, DCP David Misime leo Septemba 1,2025, msamaha huo umetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Innocent Bashungwa, kwa mamlaka aliyopewa chini ya Kifungu cha 66 cha Sheria ya Udhibiti wa Silaha na Risasi ya Mwaka 2015, Sura ya 223 na marejeo ya mwaka 2023.
DCP Misime ameeleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya juhudi ya utekelezaji wa maazimio ya Kimataifa na kikanda kuhusu udhibiti wa silaha ndogo ndogo na nyepesi, ambazo mara nyingi zimekuwa chanzo cha uvunjifu wa amani, ukosefu wa usalama,hofu kwa watu, majeruhi na vifo.
Amesemakuwa mtu yeyote atakayesalimisha silaha katika kipindi tajwa hatowajibishwa kwa hatua zozote za kisheria, lakini yeyote atakayekutwa na silaha baada ya muda wa msamaha kumalizika atachukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria.
Amefafanua kuwa usalimishaji wa silaha hizo utafanyika nchi nzima, katika vituo vya Polisi, ofisi za Serikali za Mitaa, au kwa watendaji wa kata na shehia kuanzia saa mbili asubuhi hadi saa kumi jioni.
“Pia Jeshi la Polisi linawasiistiza wananchi wote ambao ndugu zao walikuwa wanamiliki silaha kihalali na wamefariki, wahakikishe wanazisalimisha kulingana na masharti yaliyotajwa. Aidha wamiliki binafsi wa silaha zikiwemo kampuni binafsi za ulinzi ambazo zimekuwa zikiazimisha silaha kutoka au kwenda kwa watu wengine waache tabia hiyo kwani kosa la jinai,” amesema.