Na Mwandishi Wetu
Mahakama ya Wilaya ya Pangani, mkoani Tanga, Agosti 18, 2025 imetoa hukumu ya kifungo cha miaka 20 jela kwa mtuhumiwa Idd Shelugwaza (26), mkulima na mkazi wa Kijiji cha Kwakibuyu, Kata ya Kipumbwi, wilayani Pangani, baada ya kupatikana na hatia ya kosa la shambulio la aibu dhidi ya mtoto mwenye umri wa miaka minne.
Awali, ilielezwa mahakamani kuwa mnamo Juni 24, 2025 huko Kijiji cha Kwakibuyu, mtuhumiwa alitenda kosa hilo dhidi ya mtoto huyo ambaye ni mwanafunzi na mkazi wa kijiji hicho. Tukio hilo liliripotiwa katika Kituo cha Polisi Pangani ambapo mtuhumiwa alikamatwa na uchunguzi wa shauri hilo ulianza mara moja.
Shauri hilo lilifunguliwa mahakamani kwa namba 15855/2025 na kupelekwa mbele ya Hakimu Francisca Magwiza – SRM. Baada ya kusomewa shtaka, mtuhumiwa alikana kutenda kosa hilo, na shauri liliendelea kwa mashahidi mbalimbali kutoa ushahidi wao mahakamani.
Akisoma hukumu jana Agosti 18, 2025, Hakimu Magwiza alisema kuwa mahakama imeridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka, hivyo kumpata mtuhumiwa na hatia ya shambulio la aibu na kumhukumu kifungo cha miaka 20 jela ili iwe fundisho kwa jamii na kulinda haki za watoto.