Na Mwandishi wetu
MKUU wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge amesema ushirikishwaji wananchi kwenye miradi ya maendeleo unaofanywa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) ni wa mfano na unapaswa kuigwa na taasisi zingine.
Aidha, amewaomba Madiwani kutoa ushirikiano kwa DAWASA ili kuhakikisha wananchi wanatunza vyanzo vya maji na kupitia Halmashauri zao nao wanatenga fedha katika bajeti kwa kuweka kipaumbele miradi ya maji ilikupunguza tegemeo lote kwa DAWASA na kuweza kufanikisha utelekezaji wa miradi mingi ya maji.

Kunenge amesema hayo wakati akizindua rasmi ziara ya kimafunzo kwa Madiwani wa Mkoa wa Pwani ya kutembelea vyanzo vya maji na mitambo ya kuzalisha maji ili kupata uelewa wa pamoja wa hatua za uzalishaji hadi kufikisha huduma ya maji kwa wananchi.
Amesema ziara iliyoandaliwa na DAWASA ni kielelezo muhimu cha ushirikishwaji wa wananchi ili kuwa na mipango ya pamoja katika kuimarisha upatikanaji wa huduma ya majisafi.
“Niseme tu kwamba DAWASA ni mojawapo ya Taasisi ya Serikali iliyoweza kubadilika kiutendaji na kufanya jitihada kubwa katika kuboresha huduma kupitia miradi ya kimkakati.

Na sasa wanawashirikisha viongozi wa wananchi kupata uelewa wa pamoja kuhusu huduma ya majisafi kuanzia hatua ya uzalishaji hadi usambazaji kwa wananchi, hii ni hatua ya msingi katika utoaji wa huduma bora,” amesema Kunenge.
Katika ziara hiyo, Kunenge amesema DAWASA inapata fedha kutoka Serikali kuu, hivyo utatuzi wa changamoto unakuwa kwa mkakati, lakini na sisi Serikali za Mitaa katika bajeti zetu tutenge fedha kwa ajili ya miradi ya maji tusibaki kuwaachia mzigo wote DAWASA.

Awali, Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mhandisi Mkama Bwire amesema mkakati uliopo kwa sasa ni kuwashirikisha wadau muhimu wakiwemo Madiwani ambapo wameanza na Mkoa wa Pwani kwa kuwaandalia ziara na baadaye kutembelea kila Halmashauri kwa ajili ya mafunzo kuhusiana na huduma ya maji pamoja na upangaji wa vipaumbele vya kutekeleza.
Amewema kama tunavyoelewa kwa sasa mahitaji ya huduma ya maji katika Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani ni sawa na lita za ujazo milioni 772 kwa siku, wakati uwezo wa uzalishaji maji ni lita za ujazo milioni 550 kwa siku.
“Jitihada mbalimbali ikiwemo ujenzi wa miradi ya kimkakati zimeanza kutekelezwa ili kuimarisha upatikanaji wa huduma ya maji kupitia kushirikiana na wadau muhimu ambao ni madiwani.

“Serikali imekwisha toa kiasi cha Shilingi Bilioni 16.5 za ununuzi wa pampu mpya 8 kwa ajili ya kuongeza ufanisi wa uzalishaji kwenye mtambo wa kuzalisha maji Ruvu Juu na Chini, na pampu 4 zimefika tayari. Pia tumepata kibali tufanye upanunuzi wa mtambo wa uzalishaji maji Ruvu Chini kwa kuongeza uzalishaji wa maji kwa nyongeza ya lita milioni 90 kwa siku,” amesema Mhandisi Bwire.
Amebainisha kuwa, hatua nyingine ni ya ujenzi wa mradi wa mtambo wa Rufiji utakaozalisha lita za maji bilioni 1.5 kwa siku ambapo itakwenda kuondoa kabisa changamoto ya huduma ya maji na kuwa na maji ya ziada ya kutosha kuhudumia wananchi kwa kipindi chote cha mwaka.


