Na Mwandishi Wetu
WATANZANIA wametakiwa kujitokeza kwa wingi kuchangamkia fursa ya ajira iliyotangazwa na Serikali kwa kushirikiana na Kampuni ya Al-MahaTravel and Tours ambapo nafasi 1,150 za kazi ya udereva wa mabasi ya mwendo kasi zinapatikana nchini Qatar.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Al-Maha Travel, Abdallah Mohamed, alisema mchakato wa usaili utaendeshwa kwa uwazi na hautamhusisha mwombaji kugharamia fedha yoyote, huku akiwahimiza madereva wenye vigezo kujitokeza kuomba nafasi hizo kwa wakati.

Alisema waombaji wanapaswa kuwa na leseni halali ya udereva Daraja C au E, umri kati ya miaka 25 hadi 50, hati halali ya kusafiria pamoja na uwezo wa kuwasiliana kwa lugha za Kiingereza au Kiarabu.
“Aidha, waombaji wote watatakiwa kuthibitisha afya zao kabla ya kuajiriwa. Watakaofanikiwa kuchaguliwa watalipwa mshahara wa Dola za Marekani 700 kwa mwezi pamoja na marupurupu mengine ikiwemo bima ya afya, chakula na malazi bila gharama,” alisema.
Vilevile, aliongeza kuwa gharama za tiketi ya ndege zitagharamiwa na mwajiri.
Alifafanua kuwa mwisho wa kupokea maombi ni Februari 04, 2026 na usaili utafanyika kuanzia Februari 6 hadi 8, 2026, ambapo madereva 900 wanahitajika kutoka Tanzania Bara na 250 kutoka Zanzibar.



