Na Mwandishi Wetu
Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatarajia kuzindua Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha Mtera na Kusaini Mikataba ya kutekeleza mradi wa kusambaza umeme kwenye vitongoji 9,009 katika Mikoa yote Tanzania Bara.
Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy amesema hayo Jijini Dodoma leo Januari 15, 2026 katika mkutano maalum na wanahabari alipokuwa akitambulisha matukio hayo mawili yatakayoshuhudiwa na Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi ambaye atakuwa mgeni rasmi.
“Tarehe 16 Januari, 2026 Kituo cha Kupoza Umeme cha Mtera kitazinduliwa rasmi na tarehe 17 Januari, 2026 tutasaini mikataba 30 yenye thamani ya shilingi Trilioni 1.2 kwa ajili ya kutekeleza mradi mkubwa wa kusambaza umeme katika vitongoji zaidi ya 9,000,” amefafanua Mhandishi Saidy
Amebainisha kuwa Kituo cha Mtera kimejengwa kwa gharama ya sh 9.2 bilioni na Serikali ya Tanzania kupitia REA kwa ushirikiano na Serikali za Sweden na Norway.
Aidha, Mhandisi Saidy amesema REA itasaini mikataba 30 na Wakandarasi 21 wazawa na wakandarasi tisa kutoka nje ya nchi lakini wamesajiliwa nchini kwa ajili ya kutekeleza mradi huo utakaotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu ndani ya Mikoa yote Tanzania Bara.
Amewataka wananchi kuchangamkia fursa zitakazopatikana wakati wote wa utekelezaji wake ikiwemo ajira, biashara na huduma mbalimbali zitakazohitajika na pia kuhakikisha wanachangamkia kutumia umeme kuzalisha mali na kuboresha huduma za kijamii.
“Tunatekeleza maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan; mradi huu unakwenda kufungua nchi kiuchumi ni wa kipekee na mradi mkubwa kuwahi kutekelezwa na REA kwa viwango vya gharama na idadi ya vitongoji vitakavyofikiwa,” amesema.


