Na Mwandishi Wetu
MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT), Hamis Livembe, amesema mchakato wa uchaguzi wa viongozi wa jumuiya hiyo uliomalizika hivi karibuni ulikuwa wa haki, halali na uliozingatia taratibu zote, akikanusha madai kwamba uongozi uliopo umewekwa.
Akizungumza na waandishi wa habari, Livembe alisema uchaguzi huo uliendeshwa kwa uwazi na kwa mujibu wa Katiba ya jumuiya, huku akisisitiza kuwa hakuna nguvu yoyote ya nje iliyoingilia mchakato huo.
“Mchakato ulienda sawa kabisa na ulifanyika kihalali. Mimi nilikuwepo hapa miaka minne iliyopita, hivyo hakuna kitu kipya katika uongozi huu,” alisema Livembe.

Aliongeza kuwa hata katika kipindi chake cha awali cha uongozi, JWT ilikuwa ikiishauri na kuikosoa Serikali pale ilipobidi, hali inayoonesha kuwa msimamo wa jumuiya katika kutetea maslahi ya wafanyabiashara utaendelea kuwa uleule.
Wakati huo huo, Livembe aliitaka Serikali pamoja na Tume ya Maboresho ya Sheria za Kodi kutoa hadharani matokeo ya kazi iliyofanywa na tume hiyo, akisema wafanyabiashara wana hamu kubwa ya kujua mapendekezo yaliyotolewa.
Alieleza kuwa tume hiyo iliundwa na Serikali kwa ajili ya kufanya maboresho ya sheria za kodi, lakini iliongezewa muda wa kufanya kazi kutokana na kipindi cha uchaguzi.
“Sasa uchaguzi umepita, tunamuomba Rais pamoja na Tume itoe matokeo ya ile kazi. Wafanyabiashara wana shauku ya kusikia mapendekezo, hasa kuhusu kupunguza mzigo wa kodi na kuzijumlisha kodi katika kapu moja,” alisema.

Akizungumzia hali ya biashara baada ya uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 29, 2025, Livembe alisema baadhi ya wateja kutoka nchi jirani na mikoa mingine wamepungua.
Hata hivyo, alisema JWT imefanya tathmini katika masoko ya Dar es Salaam, Arusha, Mwanza na Mbeya, na kubaini kuwa hali imerejea kuwa shwari.
“Hali imetulia na usalama umedhibitiwa vya kutosha. Tunawaomba wafanyabiashara na wateja warejee kwani mazingira ya biashara yako salama,” alisisitiza.


