Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa maji, Jumaa Aweso amekagua na kujiridhisha na wingi wa Maji yanayoingia katika Mtambo wa Maji Maji Ruvu Juu uliopo Wilaya ya Kibaha Mkoani Pwani ikiwa ni ishara ya kuendelea kuimarika kwa huduma ya Maji.
Aweso amesema hatua hiyo ni jitihada zinazoendelea kutekelezwa na Serikali kupitia Wizara ya Maji na Taasisi za DAWASA na Bonde la Wami Ruvu za kuhakikisha inapambana na upungufu wa huduma ya maji iliyojitokeza katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani.
“Nimeona kazi inayoendelea niseme kwa dhati nimefarijika na inanipa imani kubwa kwamba tutavuka salama katika kipindi hiki cha mpito, niwapongeze watu wa DAWASA, Bonde la Wami Ruvu, vyombo vya ulinzi na Usalama pamoja na wadau wote wanaoshiriki kazi hii kuhakikisha inakamilika kwa wakati” ameeleza Waziri Aweso.

Amesema kuwa maendeleo ya kazi hiyo ni hatua muhimu katika jitihada za kuwapatia huduma endelevu ya maji wananchi wa Dar es Salaam na Pwani na kuendelea kuwaasa Wananchi kutumia maji kwa uangalifu na kuwa na desturi ya kuwa na vyombo vya kuhifadhi Maji.
“Tumepokea habari njema kutoka kwa wenzetu wa Mamlaka ya hali ya hewa kuwa mvua zinaanza kunyesha, na tayari katika maeneo ya Morogoro mvua imenyesha siku ya jana, nina imani kubwa tutavuka salama kipindi hiki cha mpito na hali kurejea sawa. Katika kipindi hiki tutahakikisha maji yanayopatikana yanagawanywa kwa usawa kwa kila mwananchi” amesisitiza Aweso.


