Na Mwandishi Wetu
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba amesema ni muhimu watanzania kutanguliza utu na heshima kwa familia zilizopoteza wapendwa wao, akipinga namna ambavyo baadhi ya watu wamekuwa wakichapisha taarifa au picha mtandaoni kana kwamba vifo ni jambo la kusherehekewa.
Amesema hayo wakati akijibu maswali aliyoulizwa kwenye mkutano na wahariri wa vyombo vya habari ya kutaka kujua idadi ya vifo vilivyotokea Oktoba 29, 2025 kutokana na maandamano yaliyofanyika na kusababisha vurugu.
“Tunaongelea maisha ya watu, tunaongelea watu waliopoteza wapendwa wao. Mtu amepoteza ndugu yake halafu wewe unaposti kama hafla,” amesema Waziri Mkuu, akionyesha masikitiko yake juu ya tabia ya kutafuta umaarufu kupitia misiba.


“Katika mazingira ambayo mtu amepoteza mpendwa wake mnataka tuanze kuhesabu kama majengo, magari au mafanikio? Mwingine anataja idadi licha ya kwamba hayupo hapa,” ameeleza.
Aidha Dk. Mwigulu ametaja vitu vilivyoharibiwa kutokana na vurugu hizo kuwa ni magari 1,642 ya watu binafsi yaliharibiwa, baadhi yakiteketezwa kwa moto, vituo vya mafuta 672 na bodaboda 2,268.
Amesisitiza umuhimu wa kuzingatia utulivu na amani, akibainisha kuwa Watanzania wanapaswa kuepuka fujo zinazoweza kuharibu maisha na ustawi wa kila mmoja.
Ametoa wito kwa Watanzania kuwa makini na makundi ya watu wenye nia ya kuichafua na kuiharibu Tanzania na wakatae kutumiwa kufanya uovu.
“Kila mmoja alibebe jambo hili kwa ukubwa, hawatupendi, wanaangalia rasilimali zetu, nchi yetu sio masikini, kuna watu wanamezea mate rasilimali zetu, ninawahakikishia kuwa tutailinda Tanzania na Rasilimali zake kwa gharama yoyote ile,”


