Na Mwandishi Wetu
Jeshi la Polisi nchini limekabidhiwa mashine maalumu ya kuweka alama silaha zilizopo nchini ikiwa ni hatua mbalimbali zinazochukuliwa katika kuzuia uzagaaji wa silaha ndogondogo na nyepesi ili kuepuka madhara yanayoweza kuwapata wananchi na nchi kwa ujumla.
Mashine hizo mbili zimekabidhiwa na Mwakilishi wa Taasisi ya Kikanda ya kupambana na uzagaaji wa silaha haramu na nyepesi katika Ukanda wa Maziwa Makuu na Pembe ya Afrika (RECSA), Eric Kailanga na kupokelewa na Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Zanzibar, DCP Zuberi Chembera wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya uwekaji alama na kutunza kumbukumbu za silaha kwa Askari Polisi jijini Dodoma.

Akizungumza baada ya kupokea mashine hizo, DCP Chembera amesema Jeshi la Polisi limeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuhakikisha kuwa nchi yetu inaendelea kuwa salama na kupatikana kwa mashine hizo kutasaidia kwa kiasi kikubwa juhudi hizo.
Aidha, aliwataka washiriki wa mafunzo ya uwekaji alama kuzingatia kikamilifu mafunzo watakayopata ili kuhakikisha kuwa utendaji wao unazidi kuimarika na kwenda kuwafundisha wengine ambao hawajapata fursa hiyo.

Kwa upande wake Mratibu wa Kitaifa wa Udhibiti wa Silaha ndogondogo na nyepesi nchini, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Berthaneema Mlay amesema mashine hizo mpya walizopatiwa ni za kisasa na zitaendelea kuimarisha utendaji kazi wa kudhibiti silaha haramu nchini.
Naye Mwakilishi wa kituo cha RECSA, Eric Kayiranga amesema kituo hicho kitaendelea kushirikiana na nchi wanachama katika kuhakikisha kuwa mafunzo ya mara kwa mara yanafanyika kwa lengo la kuongeza weledi kwa vyombo na taasisi zinazosimamia sheria.