Na Tatu Mohamed, Dodoma
CHUO cha VETA Singida, kimeendelea kutoa mchango mkubwa katika kuinua sekta ya mifugo nchini kwa kutoa mafunzo ya muda mfupi na mrefu kwa vijana kuhusu ufugaji bora na afya ya wanyama.
Hayo yamesemwa na Ladslous Chemele, Mwalimu wa fani ya Afya ya Wanyama na Uzalishaji kutoka chuo hicho, wakati wa maonesho ya Wakulima na Wafugaji (Nanenane) yanayoendelea jijini Dodoma.
“Tunatoa mafunzo kwa vijana kuwa wataalamu wa afya ya wanyama pamoja na uzalishaji. Hawa ni wataalamu wanaoweza kuchunguza na kutibu magonjwa ya wanyama mbalimbali wanaofugwa majumbani, wakiwemo ng’ombe, mbuzi, nguruwe pamoja na ndege kama kuku, bata, kanga, njiwa na kwale,” amesema Chemele.

Ameongeza kuwa katika maonesho hayo ya Nanenane, wafugaji wanaotembelea banda lao wanaelimishwa kuhusu mbinu bora za chanjo kwa wanyama ili kuwakinga dhidi ya milipuko ya magonjwa, pamoja na umuhimu wa kuwa na mabanda salama na yenye mazingira rafiki kwa afya ya mifugo yao.
Chemele amefafanua kuwa elimu hiyo inalenga kuwasaidia wafugaji kuongeza tija na kuhakikisha mifugo yao inakuwa na afya njema, hali itakayochangia kipato na ustawi wa kaya zao.
“Tunasisitiza pia umuhimu wa utengenezaji wa chakula bora kwa ajili ya mifugo. Wafugaji wengi hutegemea malisho ya kawaida, lakini si mara zote wanyama hupata virutubisho vya kutosha. Kwa hiyo tunafundisha namna ya kuandaa chakula kinachokidhi mahitaji ya mwili wa mnyama kwa ajili ya ukuaji na uzalishaji mzuri,” amesema.
Aidha, Chemele amewahamasisha wananchi kutembelea banda la VETA Singida katika maonesho hayo ili kupata elimu bure, huku akiwakaribisha wale wenye nia ya kujifunza kwa kina kujiunga na kozi fupi zinazotolewa chuoni.
“Mafunzo yetu ya muda mfupi hayahitaji masharti magumu. Cha msingi ni mtu kuwa na dhamira ya kujifunza na uwezo wa kujihifadhi kwa muda wa mafunzo. Hii ni fursa ya kipekee kwa vijana na wafugaji wanaotaka kufuga kwa tija na kujipatia kipato,” amesema.
Mwisho


