Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Waziri mkuu Kassim Majaliwa amesema kuwa Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa nguzo ya kuimarisha mshikamano na umoja wa kitaifa na kufanikisha maendeleo katika sekta mbalimbali za maendeleo.
Amesema kuwa katika kipindi cha uongozi wake, Rais ameweza kusimama imara katika kuendeleza miradi ya kimkakati na huduma za jamii, kusimamia demokrasia, kujenga uchumi na kuimarisha diplomasia.
Amesema hayo leo Juni 26, 2025, wakati alipotoa hoja ya kukamilisha shughuli za Bunge la 12, Bungeni jijini Dodoma.

“Sina shaka nyote mtakubaliana nami kuwa hulka yake na ustahimilivu wake umekuwa faraja kwetu sisi wasaidizi wake, watumishi wote wa umma na Watanzania wote kwa ujumla. Isitoshe, Mheshimiwa Rais wakati wote amekuwa nguzo ya kuimarisha mshikamano na umoja wa kitaifa,”
Amesema Rais Samia amekuwa mwalimu wa subira, kielelezo cha ujasiri, ustahimilivu na alama ya matumaini kwa kizazi hiki. “Ni kiongozi aliyetoa mfano wa kuwa mwanamke anaweza kuongoza hata kwenye nafasi ya Kitaifa.”
Majaliwa amesema kuwa kutokana na uongozi dhabiti wa Rais Samia, taasisi mbalimbali za kitaifa na kimataifa zimetambua mchango na maono yake katika kusimamia shughuli za kimaendeleo nchini na kuitangaza Tanzania nje ya nchi.

Ametaja tuzo za kimataifa alizopokea Rais kuwa ni Global Gates Goalkeepers, Tuzo ya Babacar Ndiaye kwa mwaka 2022, Tuzo ya Uongozi wa Kimageuzi Afrika, Tuzo ya Heshima ya Pyne Africa Awards 2022 na Tuzo ya Muongoza Watalii Bora.
Tuzo nyingine alizopata kitaifa ni Tuzo Maalum ya Heshima ya kutambua mchango wake katika kulitumikia Taifa na kuwaletea wananchi maendeleo iliyotolewa na Bunge, Tuzo Maalum ya kutambua dhamira yake thabiti ya kujenga Taifa linalostahimili Mabadiliko ya Tabianchi.