Na Mwandishi Wetu
Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Camillus Wambura amesema wanaume nchini wana haki ya kulindwa, kusikilizwa na kupewa heshima ambapo wametakiwa kutumia ofisi za Dawati la Jinsia kuripoti ukatili wanaofanyiwa majumbani.
IGP Wambura amesema hayo wakati akifungua Mradi wa Jengo la ofisi za Dawati la Jinsia na Watoto wilayani Tarime, Mkoa wa Kipolisi Tarime/Rorya ambapo jengo pamoja na samani zake limegharimu kiasi cha Sh 300 milioni ikiwa ni ufadhiri serikali ya Finland.

Aidha, IGP Wambura amewakumbusha wananchi kuwa, serikali kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali imeweza kuweka mikakati madhubuti katika kukabiliana na vitendo vya ukatili wa kijinsia na unyanyasaji dhidi ya watoto ikiwemo makosa ya ukeketaji ili kuhakikisha kuwa wanaojihusisha na vitendo hivyo wanadhibitiwa kwa kuchukuliwa hatua kali za kisheria.
Pia watendaji wa dawati hilo la jinsia wametakiwa kuhakikisha kuwa, wanatoa huduma zenye viwango kwa wateja au wahanga wa matukio ya ukatili wa kijinsia pamoja na kutafuta ufumbuzi wa kukomesha vitendo vya ukatili kwenye jamii.