Na Mwandishi Wetu
Mwanamke aitwaye Kangw’a Tungu Mahigi(25) mkazi wa Kata ya Lugubu wilayani Igunga mkoani Tabora, amefariki yeye pamoja na watoto wake wanne kwa kunywa sumu aina ya Ruruka, inayotumika kuua wadudu,
huku ikidaiwa chanzo cha vifo hivyo ikiwa ni mgogoro wa kifamilia.
Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, SACP Richard Abwao, chanzo cha tukio hilo ni ugomvi wa marehemu na mme wake baada ya mume kudaiwa kuwa na upendeleo kwa mke mdogo ambaye amemjengea nyumba ya kisasa na kumpa huduma nyingine nzuri ambazo mke mkubwa na wanawe walikuwa hawazipati.
Amesema tukio hilo limetokea June 16, 2025 ambapo mwanamke huyo alimvizia mumewe akiwa shambani kisha kununua pakiti moja ya sumu hiyo na kunywa yeye na watoto wake.
Kamanda Abwao alitaja majina ya watoto waliofariki kuwa ni Sengi James ( 8), Simon James ( 6), Elisha James ( 3) na Kashinje James (7).
Amesema kuwa mume wa marehemu anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa ajili ya uchunguzi wa kina ili kubaini mazingira halisi ya tukio hilo, ikiwa ni pamoja na nafasi yake katika muktadha wa mgogoro wa kifamilia uliokuwepo kabla ya tukio.
Kamanda huyo ameeleza kuwa nyumbani kwa marehemu ilikutwa pakiti moja ya sumu hiyo ambayo imetumika pamoja na kikombe cha plastiki chenye sumu, ambapo miili ya marehemu ili hifadhiwa mochwari Igunga kwa ajili ya uchunguzi na baadae kukabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya mazishi.
“Hili ni tendo la kikatili, kihalifu na lisilo na utu lililoangamiza maisha ya watu wasiostahili kuumizwa na pia linaondoa nafasi ya mtu mwenye matatizo kupata msaada wa kweli. Jeshi la Polisi mkoani Tabora linalaani na kuendelea kutoa wito kwa jamii, pale inapojitokeza migogoro mbalimbali kutumia viongozi wa dini, Serikali na dawati la jinsia kutafuta ufumbuzi.” amesema.