Na Mwandishi Wetu
WIZARA ya Maliasili na Utalii imebainisha vipaumbele 10 ambavyo wizara na taasisi zake zitatekeleza kwa mwaka 2025/26.
Akiwasilisha mpango wa mapato na matumizi kwa Wizara na taasisi zake kwa mwaka 2025/26, Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Dkt.Pindi Chana amesema Wizara itatekeleza majukumu yake kwa kuzingatia maeneo ya vipaumbele 10.

Amevitaja vipaumbele hivyo kuwa ni kuendelea kutangaza utalii ndani na nje ya nchi kupitia matangazo katika ligi kuu za michezo mashuhuri duniani, mashindano ya kimataifa.
Pia kupitia mashirika ya ndege, misafara ya utangazaji utalii, matamasha makubwa ya kimataifa na mitandao mbalimbali ya kimataifa na vyombo vya habari.
Dkt. Chana amesema pia kuibua na kuendeleza mazao ya utalii ya kimkakati ikiwemo maeneo ya malikale pamoja na utalii wa fukwe, mikutano na matukio, meli, michezo, tiba na utamaduni.

Pia kuboresha miundombinu ya utalii na uhifadhi ikiwemo barabara, viwanja vya ndege na huduma za utalii.Dk Chana amesema pia kuimarisha matumizi ya teknolojia za kisasa katika usimamizi wa uhifadhi na rasilimali, ufuatiliaji, utangazaji na uendeshaji wa shughuli za utalii.
Pia kuimarisha ulinzi na uhifadhi wa rasilimali za wanyamapori, misitu, nyuki na malikale na kuongeza uzalishaji na thamani ya mazao ya misitu na nyuki.Dk Chana amesema pia kuendelea kuimarisha mifumo ya upatikanaji wa takwimu mbalimbali, kufanya tafiti za kimkakati na kutoa huduma za ushauri zinazohusu masuala ya uhifadhi endelevu wa wanyamapori, misitu na nyuki, malikale na uendelezaji utalii.

Amesema vipaumbele vingine ni pamoja na uelimisha na kuhamasisha jamii kuhusu uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali za wanyamapori, malikale, misitu na ufugaji nyuki.
Pia kuimarisha usimamizi wa mifumo ya ukusanyaji wa mapato yatokanayo na shughuli za utalii na uhifadhi.Amesema pia kuandaa na kufanya Mapitio ya Sera, Sheria, Kanuni na Miongozo mbalimbali ya kusimamia na kuendeleza Sekta ya Maliasili na Utalii.